MWINGIRA AMEZAA NA MKE WANGU - MUME

TUHUMA nzito dhidi ya kiongozi wa Kanisa la Efatha, Nabii Josephat Mwingira, zimefunguliwa katika Kituo Kikuu cha Polisi (Central), Kibaha, Pwani.
Dk. William T. Morris ambaye ni daktari anayetambuliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa (UN), ndiye aliyeshusha tuhuma hizo, akidai kwamba Mwingira amezaa na mke wake, Dk. Philis Nyimbi.
Morris ambaye wasifu wake unaeleza namna sifa zake zinavyojipambanua ndani ya Shirika la Afya Duniani (WHO), aliwasilisha madai hayo mwaka 2011, akitaka jeshi la polisi limsaidie kupata haki zake.
 JALADA LA UCHUNGUZIMtandao mpana wa mitego ya habari  uliwezesha kunasa uwepo wa jalada la uchunguzi, likiwa na nambari KBA/ PE/23/2011 ambalo mhusika wake ni Mwingira.
Shauri hilo linasomeka kwenye kumbukumbu za jeshi la polisi KBA/ PE/23/2011 JALADA LA UCHUNGUZI.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Pwani, ACP Unrich Matei, alilithibitisha kwamba kweli jalada hilo lilifunguliwa na tuhuma zake ni hizo za Morris kudai Mwingira amezaa na mkewe.

UTHIBITISHO WA BARUA YA POLISI
Habari zinasema kuwa Morris alipofungua shauri hilo, haikuchukua muda mrefu alirudishiwa majibu kwamba tuhuma zake azipeleke mahakamani kwa sababu hazina mashiko katika jinai.
Awali, tuhuma zake zilijipambanua kwamba Mwingira amekuwa na uhusiano usiofaa na mkewe (Philis) mpaka kumpa ujauzito na hatimaye mtoto akazaliwa.

Katika barua hiyo, iliyosainiwa na aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi wa Jinai (RCO), Mkoa wa Pwani, SSP E.H. Mwijage, ilimwelekeza Morris kutafuta haki katika mkondo mwingine wa sheria, hususan mahakamani.
Barua hiyo ilikuwa na kichwa; YAH: KBA/PE/23/2011, KOSA: JALADA LA UCHUNGUZI, MTUHUMIWA: JOSEPHAT MWINGIRA.

Vilevile barua hiyo, ilikuwa na kumbukumbu nambari PWA/CID/130/VOL XXV11/211 na ilikuwa ni majibu ya ile ambayo Morris alimwandikia RCO, Desemba Mosi, 2011.
Barua hiyo ya RCO, iliandikwa Januari 25, 2012 ikiwa na maelezo yafuatayo;

“Baada ya uchunguzi makini juu ya malalamiko yako, uchunguzi umebaini kuwa kosa lililofanyika ni adultery (kuzini) au defamation (udhalilishaji) ambapo katika sheria za makosa ya jinai, makosa hayo hayapo.
“Kutokana na sababu hizo hapo juu, tunakushauri uchukue hatua nyingine za kupata haki yao au ufungue kesi ya madai mahakamani dhidi ya mtuhumiwa.”

MORRIS ANASEMAJE?
Morris alitafutwa na waandishi wetu na alipopatikana, alikiri kila kitu lakini alidai kwamba amekuwa akipata shida kufungua kesi ya madai mahakamani kutokana na misukosuko mbalimbali anayopewa.
Alisema, yeye siyo Mtanzania na kutokana na hilo, amekuwa akisumbuliwa na hata kutishiwa kurudishwa kwao.
Aliongeza kwamba ameendelea kushughulikia hili suala lake kwa utulivu bila papara ili asipoteze haki zake za msingi.

UMOJA WA MATAIFA
Kwa upande mwingine, zipo nyaraka ambazo Morris inadaiwa alizituma Umoja wa Mataifa kwa barua pepe (tunayo nakala yake) aliyoielekeza kwa katibu mkuu wa shirika hilo, Ban Ki Moon, Januari 11, 2011.
Hata hivyo, ndani ya barua hiyo, Morris ameeleza tuhuma nyingine mbalimbali kuhusu Mwingira lakini zinahifadhiwa kwa sasa.

Katika barua hiyo, Morris aliomba ulinzi kwa sababu tayari Ubalozi wa Marekani nchini, Umoja wa Ulaya, Shirika la Kimataifa la Haki za Binadamu (Amnesty International), Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na taasisi ya haki za binadamu nchini, ameshazipa taarifa.
Aidha, Morris alimsisitizia Ki Moon ombi lake la kusaidiwa kupata haki zake na mkewe pamoja na madai mengine aliyoyaandika katika waraka huo.


CHETI CHA NDOA
Kwa mujibu wa Morris, Philis ni mke wake halali, aliyefunga naye ndoa takatifu katika Kanisa la St. Alban jijini Dar es Salaam, Desemba 23, 2001, akiwa na umri wa miaka 39 na mkewe wakati huo alikuwa na miaka 30 na kupewa cheti cha ndoa namba B. 0638572 na ilifungishwa na Padri Canon William Kambanga.linayo nakala ya cheti hicho cha ndoa.

MKE NAYE AZUNGUMZA
Kuhusu tuhuma hizo, Philis alisema kuwa Mwingira hahusiki kwenye matatizo yao.
“Yule alinitelekeza, siyo mume wangu,” alisema Philis na kuongeza: “Angekuwa mume kweli asingenitelekeza na kunisaliti mpaka kwa mtoto wa kike ambaye tunaweza kumzaa.”
Aliongeza kuwa alimvumilia Morris kwa mambo mengi na hawezi kumsamehe kwa sababu alimuumiza sana.

MWANDISHI: Kwa maana hiyo unakiri kwamba ulizaa na mwanaume mwingine?
PHILIS: Ni kweli, nilifanya hivyo baada ya yeye kunitelekeza na hakuwa na uwezo wa kunizalisha.
MWANDISHI: Huyo mwanaume ni nani? Ni Mwingira?
PHILIS: Hilo swali siwezi kujibu, iwe Mwingira au mwanaume mwingine yeyote, labda kwa wakili wangu au mahakamani.
MWANDISHI: Unafahamiana na Mwingira kwa ukaribu?
PHILIS: Ndiyo nafahamiana naye, ni ndugu yangu.

MWANDISHI: Ndugu yako kivipi? Labda kaka, mjomba au?
PHILIS: Wewe elewa ni ndugu yangu, ila kuhusu ndugu yangu kivipi, hilo swali siwezi kukujibu.
MWANDISHI: Umewahi kuwa muumini wa Mwingira?
PHILIS: Iwe nasali RC, KKKT au vyovyote vile, wewe inakuhusu nini?
MWANDISHI: Kama utasuluhishwa na Morris, unaweza kuishi naye tena?
PHILIS: Wewe kaka, hivi unajua jinsi yule mwanaume alivyoniumiza? Siwezi kabisa.

KUMPATA MWINGIRA SHUGHULI
Waandishi wetu walifanya jitihada za kuzungumza na Mwingira mara tatu bila mafanikio.
Mara ya kwanza, waandishi wetu walikutana na walinzi ambao walisema, hawataonana na Mwingira, isipokuwa wakutane na msaidizi wake ambaye anaitwa Mchungaji Urasa.
Mara ya pili, waandishi wetu walikutana na Urasa ambaye alisema ili kumuona Mwingira inabidi kuandika nambari ya simu, jina na mahali ambako wanatoka.

Mmoja wa waandishi wetu aliacha jina, nambari ya simu na maelezo mengine yaliyohitajika lakini hakupata majibu yoyote.
Jumapili iliyopita, waandishi wetu walirudi kanisani Efatha kwa mara ya tatu na kukutana na mtu anayeitwa Samuel Peter ambaye alijitambulisha kama mtumishi.

Waandishi wetu walipomuomba Samuel awape muongozo wa kuonana na Mwingira, alijibu: “Siyo rahisi kumuona nabii.”
Hata waandishi wetu walipoomba nafasi ya kuonana na Urasa ili kukumbusha ahadi ya mwanzo, Samuel alijibu: “Hata Urasa hamuwezi kumuona, mbona huwa hamji kuripoti habari za ukombozi kama misukule? Hamuwezi kuwaona wote hao.”

KAMANDA WA POLISI
Jumapili iliyopita, Kamanda Matei, alipoulizwa kuhusu maendeleo ya kesi hiyo ya Morris na Mwingira, alisema anahitaji mlalamikaji aende ofisini kwake.
“Ni kweli tukio hilo lipo kituoni lakini jalada lake likafungwa. Naona mazingira ya kulifunga lile jalada hayakuwa sahihi, nahitaji aje ofisini kwangu tuone nini hasa kilisababisha lile jalada la uchunguzi likafungwa,” alisema Matei.

Alifafanua kuwa kesi hiyo ilifunguliwa wakati Pwani ikiwa na kamanda mwingine, kwa hiyo yeye amelikuta shauri hilo.
“Unajua yale ni madai tu, inabidi mlalamikaji aje atupe ushirikiano, mtoto apimwe damu kwa ajili ya DNA, vile vinasaba ndivyo vitatoa jibu yule mtoto ni wa nani,” alisema Kamanda Matei.

0 comments:

Post a Comment

 
Design by Jambo Tz